PASIPOTI YA GAIDI - Kitabu Cha 1

By: Richard Mwambe

0
Available Stock:

Hujuma Na Uzandiki

 

 

Mwandishi: Richard MWAMBE

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

SURA YA I

 

IKULU – DAR ES SALAAM

Saa 10:30 alfajiri

 

W

AKATI giza likijiandaa kutoweka na kuipisha nuru ya asubuhi, miti yote ilikuwa imetulia kana kwamba kuna aliyeiambia ifanye hivyo. Ni Tausi mmoja mmoja aliyekuwa akilia alfajiri hii tena kwa nyakati tofauti. Hawakuwa na zamu ya kufanya hivyo isipokuwa ilitokea tu, ndivyo walivyoumbwa.  Hawakuwa wakijua lolote linaloendelea katika maisha ya mwanadamu wakati huo, zaidi walisubiri kukuche waendelee kupendezesha mandhari ya eneo hilo. Hawa walikuwa kivutio kikubwa sana katika eneo hilo kwa wapiti njia.

Hekaheka katika jengo hilo la Makao Makuu ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilikuwa kubwa. Vijana wa jeshi la polisi, kikosi maalum cha kutuliza ghasia, walikuwepo wakiwa kimejiweka tayari kwa lolote, ijapokuwa huwa hapo kwa lindo kila siku lakini leo hii walikuwa kivingine kabisa. Mbali na wao, eneo hilo, afajiri hiyo lilizungukwa pia na vijana wa Jeshi la Wananchi waliovalia kombati zao za mabakamabaka, wakiwa na silaha nzitonzito mikononi mwao, kila mmoja akionekana kutingwa na shughuli inayompasa kufanya kwa muda huo. Magari ya wagonjwa kutoka Jeshi la Wananchi yalikuwa yikifanya kazi ya kubeba majeruhi na maiti zilizokutwa ndani ya jengo hilo, hekaheka.

Katibu Mkuu kiongozi akasimama katikati ya ukumbi mkubwa ndani ya jengo hilo, alikuwa kimya bila kusema lolote. Macho yake yalijawa na machozi, midomo yake ilibaaki ikimwemwesa.

“Samahani Mzee!” sauti ilisikika kutoka nyuma yake, alishtuka kama mtu aliyekutana ghafla na mtoa roho, akageuka na kumtazama kijana aliyemwita. Mzee huyo alijikuta anashindwa hata kuitikia ile salamu au kuuliza anamwitia nini, badala yake alimfuata yule kijana pindi alipoondoka eneo lile. Moja kwa moja walifika kwenye ukumbi mdogo ambao ulikuwa na watu wasiozidi sita, yaani wale wenye vyeo vya juu, wenye dhamana ya ulinzi na usalama wa nchi, pamoja nao kulikuwa na wasaidizi wengine ambao ni maofisa wachache wa Ikulu. Akaketi katika kiti kilichokuwa wazi, akiwatazama watu hawa kwa zamu, pamoja nao alikuwapo mtu mwenye cheo cha pili kutoka kile cha mkuu wa nchi.

“Kama mnavyoona… maofisa kadhaa na wafanyakazi wa Ikulu wameuawa,” Makamu wa Rais aliliambia jopo, “kilichotokea hapa hakieleweki, hakuna anayejua nini kimetokea, ila mke wa Rais yaani First Lady ametoweka, nafikiri, kwa uwazi kabisa kuwa huu ni uvamizi lakini sijui ni nani au siwezi kuhusisha na kikundi gani kwani uchunguzi ndio kwanza umeanza,” akatulia kimya bila kusema lolote. Macho yake yalionekana wazi kutona kwa machozi ambayo hayakutaka kumwagika.

“Bila shaka, inawezekana walidhamiria kumteka au kumdhuru Rais mwenyewe, walipoona hayupo basi wameondoka na mkewe, First Lady. Kumbukeni, Ikulu ya Tanzania ni kati ya majengo machache duniani yanayolindwa kwa mitambo ya hali ya juu na wanausalama waliokomaa kwenye fani yao, lakini kama tumevamiwa, bila shaka, waliyovamia ni kundi lenye weledi wa juu zaidi katika medani hii ya usalama,” waziri wa ulinzi aliongezea na wajumbe wote wakatikisa vichwa.

“Tumepoteza vijana wetu makini kabisa ambao waliaminiwa sana na mkuu. Taarifa nimeshamfikishia, na amekatisha ziara yake, anarudi nyumbani kwani hali hii si ya kuvumilika, tunategemea neno la mwisho kutoka kwake,” Makamu akalieleza baraza na wote wakaunga mkono.

“Mheshimiwa Makamu, naomba utoe tamko la wazi kwa sasa juu ya hali hii, maana, tusipoangalia, waandishi wa magazeti kama kawaida yao wataanza kutoa habari zisizothibitishwa,” msemaji wa Ikulu alimwambia Makamu wa Rais.

“Ok, naomba ieleweke hivi, Ikulu imevamiwa na kundi la kigaidi, walinzi kadhaa wameuawa na bado kuna hali ya sintofahamu. Vyombo vya usalama viko katika harakati za kuhakikisha vinategua kitendawili hiki ndani ya saa chache. Tunaomba wananchi kuwa watulivu na pia kutoa taarifa polisi pindi unapoona mtu unayemhofia katika maeneo yenu,” makamu wa Rais akazungumza. Punde tu taarifa ile ikachapwa katika mashine na kusainiwa akakabidhiwa huyo bwana, Msemaji wa Ikulu ili kuwafikishia wanahabari waliofika alfajiri hiyo katika ukumbi mdogo wa maelezo ulio ndani ya jengo hilo.

Ikulu ilikuwa haiingiliki mpaka uwe na kibali maalumu, vijana wa Jeshi la Wananchi waliegesha magari yao upande wa baharini na mengine mawili upande wa hospitali ya Ocean Road na nyingine zilisimama karibu na Ofisi ya Hazina. Barabara ya Magogoni ilifungwa haikuruhusiwa gari wala mtembea kwa miguu kupita eneo lile. Juu angani helkopta ya jeshi na polisi zilikuwa zikifanya doria zikishirikiana na zile za Jeshi la Wananchi.

Kwa ujumla jiji la Dar es salaam lilikuwa katika misukosuko ya hapa na pale. Majira ya saa sita mchana barabara kubwa na ya muhimu zaidi katika jiji hilo ilifungwa kwa muda, ile inayotoka uwanja wa ndege kuelekea mjini. Ving’ora vikasikika na gari kama saba hivi zilipita kwa kasi ya ajabu kuelekea mjini. Na dakika kumi na mbili tua gari hizo ziliingia katika lango kuu la Ikulu na kuegeshwa mahala pake wakati tayari Mkuu wa nchi alikuwa amekwishashuka na kuingia ndani ya jengo hilo, moja kwa moja akiwa na walinzi wake alipitiliza na kuteremka ngazi iliyompeleka katika chumba maalum ambacho hufanyia mikutano yake ya siri kilichopewa jina la ‘Kilimanjaro Square’.

“Nimesikitishwa na kilichotokea, hii haiwezekaniki kuivumilia, ni uvamizi,” Rais aling’aka huku akizunguka chumba badala ya kuketi chini. Watu watano waliokuwa naye ndani ya chumba hicho walibaki kimya kabisa. Mkuu wa nchi akarudi na kuketi mezani kwake, akakamata kalamu yake na kutaka kuandika kitu lakini mkono ulikuwa mzito.

“Tulikuwa tunakusubiri wewe Mheshimiwa Rais ili utoe neno lako vijana waingie kazini mara moja,” Makamu wa Rais alitamka.

“Oh! Shiiit, Come on, hii ni Cold War! Let me say Cold War, na ntaipigana mpaka mwisho. Mtu kukuvamia ndani ya chumba chako na kumchukua mkeo ni matusi, matusi yasiyovumilika!” akang’aka huku akisimama wima kwa hasira, “Ni jengo gani au taasisi gani Afrika ina ulinzi mkali na makini kama hili jengo hapa? Hakuna, ninyi mnajua na dunia inajua. Sasa hawa waliokuja na kufanikiwa kufanya madhara haya ina maana wamejuaje njia za kuingia humu na njia za kutokea kama si hujuma?” aliendelea kung’aka kwa sauti. Kisha akatulia kidogo huku kijasho kikimtiririka, mwili wake ulimtetemeka kama mtu asikiaye baridi kali. Akasimama na kutazamana na Mkuu wa Majeshi “Nataka vijana wako waliobobea kweye michezo hii wahakikishe wanampata First Lady ndani ya saas12.

“Umesomeka Amiri Jeshi Mkuu,” akajibu mkuu wa majeshi na kusimama akatoa saluti ya utii.

“Na ninyi wengine muwe katika kazi zenu za kawaida lakini nyote muangaze macho katika sakata hilo,” akatoa maagizo kwa viongozi wa vikosi vingine. Nao wakaitikia wito huo na kila mmoja akaondoka katika jengo hilo lililotukuka. Ni dakika hiyohiyo tu ambapo ule ukumbi ulikuwa na watu wawili tu yaani Rais na Makamu wake.

“Inaniuma sana Mheshimiwa!” Rais alimwambia makamu wake huku mikono yake ikiwa haitulii sehemu moja.

“Mimi pia, ukizingatia tumepoteza vijana wenye ujuzi wa hali ya juu sana katika maswala ya usalama,” makamu naye alijibu.

“Nina uhakika kwa vijana wetu hawa wa JW, hao wahalifu watapatikana tu,” Rais akajibu.

“Sawasawa kabisa, lakini unafikiri wao peke yao wataweza kulibaini kundi hilo lililofanya kadhia hii?”

“Kwa nini unasema hivyo?”

“Kwa sababu kutokana taaluma yao nahisi kama kazi hii inaweza kuwa ngumu,” makamu alikazia.

“Hapana! Hata mimi nilikuwa mwanajeshi, najua, tuna idara ya upelelezi ya jeshi, na kutokana na uzito wa jambo hili, wao ndio watu muafaka.” Akameza mate kisha akaendelea, “Unajua hawa lazima wapambane na mtu anayelingana nao kwa sababu bila shaka ni magaidi sasa gaidi ni levo nyingine, lazima apambane na mtu wa levo yake na hao si wengine ni vijana wa jeshi,” Mheshimiwa Rais alamwelekeza makamu wake juu ya mpango huo. Kikao cha wawili hao kilipomalizika, Makamu wa Rais akaondoka na kumwacha mkuu wake peke yake ndani ya ofisi hiyo. Kitendo tu cha Makamu wa Rais kutoka na kumwacha mheshimiwa peke yake, simu ya mezani ilianza kuita kwa nguvu na fujo. Mheshimiwa Rais akaingalia kwa tuo kabla hajaamua kama ainyanyue na kuisikiliza au aiache, lakini tatizo ni kwamba hakujua simu hiyo ilikuwa inahusu nini au inamhusu nani. Na mara nyingi simu ya chumba hicho ikiita basi huwa kunakuwa na jambo zito la kiofisi. Kwa mkono wa kitetemeshi aliukwanyua mkono wa simu ile na kuiweka sikioni bila kuongea lolote.

“Usijaribu kuchukua hatua yoyote kwa kumtafuta mkeo, tunajua unampenda na ndiyo maana tumemchukua, lakini ujue sisi tunachokitaka si fedha wala hatuna ugomvi na wewe. Tunahitaji jambo moja tu, toa amri ya kuondoa majeshi yako ya kulinda amani katika Kusini mwa nchi ya Ngoko. Ukilitekeleza hilo, mkeo utampata, na husipotekeleza tutateka na watu wa familia yako waliobakia, na wewe utakuwa wa mwisho…”....


NB: Riwaya hii ina mfululizo wa vitabu vinne; 1. Hujuma na Uzandiki, 2. Double Agent, 3. Anguko la Kizito na 4. Kazi Nzito

Ukitaka vitabu vinaavyofuata, tafadhali ingia kwenye huduma ya malipo kwa kuchagua category ya NUNUA KITABU 

View or Download Book
📘 View PDF ⬇ Download

Related Products

Product Image
MKATABA WA KIFO (Jiue Mwenyewe)

By: richard MWAMBE

Product Image
ISABELA - Mpango Hasi

By: Richard R. Mwambe

Product Image
KIJASHO CHEMBAMBA - EP 01

By: Richard Mwambe

Product Image
KITANZI CHA MWISHO

By: Richard Mwambe